Friday, October 21, 2011

Lindi watekeleza miradi ya maendeleo

HALMASHAURI  ya manispaa ya  Lindi,  imetumia  zaidi ya Sh4 bilioni  kugharimia  miradi mbalimbali ya  maendeleo  katika kipindi cha Julai 2010  hadi Juni 30 mwaka 2011. Hayo yalielezwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo, Ahmad Sawa , wakati akitoa taarifa za  mapato na matumizi kwenye Kikao cha Baraza la Madiwani kilichofanyika kwenye ukumbi wa DDC mjini humo jana. Sawa, alisema katika kipindi cha  mwaka wa fedha  2010/11  Halmashauri  ya Manispaa hiyo  ilikadiriwa  kukusanya  Sh7.6 bilioni kutoka kwenye  vyanzo vya ndani  na ruzuku ya serikali kuu,  hadi kufikia  Juni 30, 2011, lakini kutokana na matatizo mbalimbali imeshindwa kufikia lengo la kufanikiwa kukusanya Sh5.2 bilioni  sawa na asilimia 79.46. Aidha Mkurugenzi wa Manispaa huyo alisema kuwa, halmashauri ilikadiria makusanyo ya ndani yatakuwa  Sh5.2 bilioni na kufanikiwa kukusanya Sh4 bilioni ambayo ni sawa na asilimia 87, na makusanyo kutoka Serikali kuu ilikadiriwa kuwa Sh4.2 bilioni ikiwa ni asilimia 72.34. Sawa alisema kwa kipindi hicho halmashauri hiyo imetumia Sh4.9 bilioni ambayo ni sawa na asilimia 65 ikiwa fedha kutoka  mfuko wa vyanzo vya ndani . Alisema kuwa jumla ya Sh3.3 bilioni fedha za ruzuku kutoka serikali kuu zimetumika ikiwa ni sawa na  asilimia 84.58, huku mapato kutoka  kwenye miradi  mbalimbali ya maendeleo imetumia Sh1.2 bilioni sawa na asilimia 60.08 na kufanya jumla kuu ya matumizi hayo kuwa ni Sh4.9 milioni sawa na asilimia 65 ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwenye manispaa hiyo. Sawa alisema  mapato ya ndani  yanaendelea kuongezeka  na kuimarika  kutoka  Sh3.8 bilioni katika kipindi cha mwaka 2008/09 hadi kufikia Sh5.6 bilioni kwa mwaka 2009/10 ikiwa ni  ongezeko  la Sh1.8 bilioni sawa na asilimia 32. Aidha Mkurugenzi huyo alisema kuwa kwa mwaka wa fedha 2011/12 mapato ya ndani yataendelea  kuimarika  kwa kuwa  kuna ongezeko la kata  tano zenye  vyanzo  vizuri vya mapato zilizohamishwa kutoka wilaya ya  Lindi kuingia manispaa hiyo.
Chanzo - Mwananchi

No comments:

Post a Comment